Yesu alipoyaona makundi ya watu, alipanda mlimani, akaketi. Wanafunzi wake wakamwendea,
2
naye akaanza kuwafundisha:
3
"Heri walio maskini rohoni, maana ufalme wa mbinguni ni wao.
4
Heri walio na huzuni, maana watafarijiwa.
5
Heri walio wapole, maana watairithi nchi.
6
Heri wenye njaa na kiu ya kufanya atakavyo Mungu, maana watashibishwa.
7
Heri walio na huruma, maana watahurumiwa.
8
Heri wenye moyo safi, maana watamwona Mungu.
9
Heri wenye kuleta amani, maana wataitwa watoto wa Mungu.
10
Heri wanaoteswa kwa sababu ya kufanya atakavyo Mungu, maana ufalme wa mbinguni ni wao.
11
"Heri yenu ninyi watu wakiwatukana, wakiwadhulumu na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa ajili yangu.
12
Furahini na kushangilia maana tuzo lenu ni kubwa mbinguni. Hivyo ndivyo walivyowadhulumu manabii waliokuwako kabla yenu.
13
"Ninyi ni chumvi ya dunia! Lakini chumvi ikipoteza ladha yake itakolezwa na nini? Haifai kitu tena, ila hutupwa nje na kukanyagwa na watu.
14
"Ninyi ni mwanga wa ulimwengu! Mji uliojengwa juu ya mlima hauwezi kufichika.
15
Wala watu hawawashi taa na kuifunika kwa chungu, ila huiweka juu ya kinara ili iwaangazie wote waliomo nyumbani.
16
Vivyo hivyo, ni lazima mwanga wenu uangaze mbele ya watu, ili wayaone matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni."
17
"Msidhani ya kuwa nimekuja kutangua Sheria ya Mose na mafundisho ya manabii. Sikuja kutangua bali kukamilisha.
18
Kweli nawaambieni, mpaka hapo mbingu na dunia zitakapopita, hakuna hata nukta moja au sehemu ndogo kabisa ya Sheria itakayoondolewa, mpaka yote yametimia.
19
Basi, yeyote atakayevunja hata amri moja ndogo kuliko zote, na kuwafundisha wengine wafanye hivyo, huyo atakuwa mdogo kabisa katika Ufalme wa mbiguni. Lakini yule atakayezishika na kuwafundisha wengine, huyo atakuwa mkubwa katika Ufalme wa mbingu
20
Ndiyo maana nawaambieni, wema wenu usipozidi ule wa Mafarisayo na walimu wa Sheria, hamtaingia kamwe katika Ufalme wa mbinguni.
21
"Mmekwisha sikia ya kuwa watu wa kale waliambiwa: Usiue! Atakayeua lazima ahukumiwe.
22
Lakini mimi nawaambieni, yeyote anayemkasirikia ndugu yake, lazima ahukumiwe. Anayemdharau ndugu yake atapelekwa mahakamani. Anayemwita ndugu yake: Pumbavu atastahili kuingia katika moto wa Jehanamu.
23
Basi, ukipeleka sadaka yako mbele ya madhabahu na hapo ukakumbuka kwamba ndugu yako ana ugomvi nawe,
24
iache sadaka yako mbele ya madhabahu, nenda kwanza ukapatane na ndugu yako, ndipo urudi ukatoe sadaka yako.
25
"Patana na mshtaki wako upesi mkiwa bado njiani, kwenda mahakamani. La sivyo, mshtaki wako atakukabidhi kwa hakimu, naye hakimu atakukabidhi kwa askari, nawe utafungwa gerezani.
26
Kweli nakwambia, hutatoka humo mpaka umemaliza kulipa senti ya mwisho.
27
"Mmesikia ya kuwa watu waliambiwa: Usizini!
28
Lakini mimi nawaambieni, atakayemtazama mwanamke kwa kumtamani, amekwisha zini naye moyoni mwake.
29
Basi, kama jicho lako la kulia linakukosesha, ling'oe ukalitupe mbali. Afadhali zaidi kwako kupoteza kiungo kimoja cha mwili wako, kuliko mwili wako wote kutupwa katika moto wa Jehanamu.
30
Na kama mkono wako wa kulia unakukosesha, ukate ukautupe mbali. Afadhali zaidi kupoteza kiungo kimoja cha mwili, kuliko mwili wako wote uende katika moto wa Jehanamu.